Home » Wito watoto washirikishwe kwenye mipango ya maendeleo – Taifa Leo
News

Wito watoto washirikishwe kwenye mipango ya maendeleo – Taifa Leo

[ad_1]

NA MASHIRIKA

Waswahili wana maneno maarufu sana wanayopenda kuyatumia wakati wanapowazungumzia watoto, kwamba “watoto ni taifa la kesho”, na “watoto ni watu wazima wa kesho”. Maneno yote haya yanaashiria umuhimu wa watoto kukuzwa vyema na kuanza kuandaliwa mapema sana.

Ikiwa dunia inaelekea kuadhimisha siku ya mtoto ambayo ni Juni Mosi, China imekuwa ikiimarisha mifumo yake ya kuwasaidia watoto wasio na ulinzi yaani wasioweza kushughulikiwa na wazazi wao pamoja na watoto walemavu na kuwahakikishia usalama zaidi watoto wote katika makuzi yao.

Hivi karibuni, Baraza la Taifa la China liliidhinisha rasmi ujenzi wa Mfumo wa Vituo vya Kuwezesha Watoto Wenye Ulemavu Kuishi maisha ya Kawaida, kwa nia ya kusaidia watoto walemavu wengi zaidi. Kwa sasa nchini China kuna watoto wenye ulemavu takriban milioni 1.67 ambao wana umri wa miaka sita au chini ya hapo.

Ingawa huko nyuma miradi mingi ya kuwawezesha watoto walemavu kuishi maisha ya kawaida, haikujumuishwa kwenye vifurushi vya bima ya afya iliyopo sasa, na kupelekea changamoto kubwa kwa watoto hao waliopo kwenye vituo va ustawi wa jamii na familia zilizo katika mazingira magumu wakati linapokuja suala la malipo ya gharama za matibabu.

Lakini sasa watoto hawa wamepata mwanga wa matumaini, kwani watapatiwa vifaa na kupewa mafunzo ili kuboresha hali zao na kuwawezesha kuishi maisha ya kujitegemea na kushiriki kwenye shughuli za kijamii pia.

Mabadiliko ya mifumo kwenye vituo hivi yataanza Oktoba Mosi mwaka huu, ambapo mwanzo vitapanua njia za msaada wa kitaasisi na kijamii kwa watoto walemavu kote nchini.

Wakati juhudi za kuwapatia maisha mazuri watoto wote wa China zikiendelea, mwaka jana zaidi ya watu milioni 12 walipewa posho za kujikimu kimaisha na watu milioni 14 wakipatiwa mafao ya ulemavu.

Kutokana na juhudi zote hizo za kuwatupia macho watoto, hivi majuzi tu Shirika la Save the Children lilitoa ripoti kwamba sasa China ni nchi namba moja ya Asia ambayo watoto wake wana makuzi bora kwa miaka miwili mfululizo, huku ikiendelea kupiga hatua katika ustawi wa watoto hao.

Ripoti hiyo ambayo imezipanga nchi kulingana na mahali ambapo watoto hawapo kwenye hatari kubwa, China ipo kwenye nafasi ya 40 ikiwa nyuma ya Marekani kwa nafasi chache tu ambayo ipo nafasi ya 36 na Russia 37.

Watoto wa China sasa wapo salama zaidi kati ya mataifa yote ya Asia, ambapo pia nchi hii imepiga hatua kubwa kwenye uchumi na kuboresha ustawi wa watoto katika miaka ya hivi karibuni. Hatua hizo ni pamoja na kuwaandikisha watoto wenye ulemavu shuleni na kuwapatia lishe bora.

Kwa upande wa Afrika siku hii huadhimishwa Juni 16 ikiwa na lengo la kuangalia maslahi mapana ya watoto ambapo umekuwa ukitolewa wito kwa watu wazima na serikali kujitolea kwa hali na mali kushughulikia changamoto nyingi zinazowakabili watoto katika Afrika.

Tunafahamu kwamba watoto wanapaswa kulindwa dhidi ya ukatili na unyama wanaotendewa ndani na nje ya familia zao. Lakini suali la kujiuliza ni kwamba je, watoto hawa wanalindwa kweli dhidi ya vitendo hivyo?

Kumekuwa na matukio mengi sana yanayowafanya watoto wajihisi kwamba hawapo salama. Bila ya kujali maisha na hatma ya mtoto, baadhi ya wazazi wamekuwa wakiwaozesha watoto wao wakiwa wangali wadogo kabisa, na kibaya zaidi ni kwamba baadhi ya watoto hawa kupachikwa ujauzito wakiwa bado hawajitambui na hata hawajafikisha umri wa miaka 10. Ni jukumu letu wazazi kuhakikisha usalama wa watoto wetu na kuwapatia mahitaji yao ya msingi kwa wakati.

Waswahili wanasema mtoto umleavyo ndivyo akuavyo, kama utamlea kuwa na utashi wa kujijengea maisha bora, basi bila shaka atafanikiwa kuwa na maisha bora.

Lakini mbali na hapo serikali za nchi mbalimbali nazo pia zina mkono wake kwenye hili. Zinapaswa kuhakikisha sheria za kuwalinda watoto zinatekelezwa, lakini kubwa zaidi ni kuhakikisha ustawi wa watoto hawa. Mbuyu ulianza kama mchicha na hatimaye ukakua na kustawi kwa kumwagiliwa mbolea na kusafishwa, watoto nao wanahitaji kuenziwa na kuangaliwa vyema ili wawe taifa bora la kesho.

CRI

[ad_2]
Source link